Papa na Sheikh Nasaruddin Umar, imamu mkuu wa Msikiti wa Istiqlal wa Jakarta, walitia saini tamko la pamoja la kutaka kuwepo kwa urafiki wa dini mbalimbali, kuchukua msimamo dhidi ya unyanyasaji wa kidini na kuhimiza hatua za pamoja za kulinda sayari ya dunia.
Papa huyo mwenye umri wa miaka 87 alikutana na Sheikh Nasaruddin kwenye msikiti huo, ambao ni mkubwa zaidi Kusini Mashariki mwa Asia, katika siku ya tatu ya ziara yake nchini Indonesia, ikiwa ni hatua ya awali ya ziara ya wiki mbili ya eneo la Asia Pasikific, ambayo pia itampeleka Papua New Guinea, Timor ya Mashariki na Singapore.
Sheikh Nasaruddin, 65, alisema kuwa tamko hilo lilikuwa na malengo mawili: "La kwanza... ubinadamu ni mmoja tu, hakuna rangi. La pili, jinsi ya kuokoa mazingira yetu.
Akifungua hotuba yake katika msikiti huo, Papa Francis alisisitiza hali ya ukuruba wa dini, akisema kwamba "kwa kuangalia kwa undani ... tunagundua kwamba sisi sote ni ndugu, wote tuko katika safari ya kidini ya kuelekea kwa Mwenyezi Mungu, zaidi ya kile kinachotutofautisha".
Alionya dhidi ya utumiaji wa dini kama silaha ya kuchochea migogoro na pia alitaja mzozo wa mazingira kama tishio lililopo kwa ustaarabu wa binadamu.
Papa alikaribishwa msikitini na bendi ambayo mara nyingi hutumika katika sherehe za Kiislamu na mara baada ya kuketi, yeye na Sheikh Nasaruddin walisikiliza aya za Qur’ani Tukufu zilizosomwa na msichana mdogo mwenye ulemavu wa macho. Aidha walisikiliza kifungu wa cha Biblia.
Msikiti wa Istiqlal uko kando ya kanisa kuu la Jakarta, na majengo hayo mawili yameunganishwa kwa na "handaki la urafiki" kama ishara ya udugu wa kidini. Papa Francis alitembelea handaki hilo kabla ya mkutano.
3489778